Page 1 of 1

NASA yapanga kujenga kituo cha utafiti mwezini

Posted: Wed Mar 25, 2026 1:05 pm
by webmaster
Shirika la anga za juu la Marekani NASA linaendelea kuubadilisha mpango wake wa utafiti wa mwezi na linapanga uwepo wa kudumu wa binadamu mwezini. Akizungumza mjini Washington, Msimamizi wa NASA Jared Isaacman amesema kuwa muda unayoyoma katika ushindani huu wa madola yenye nguvu, na mafanikio au kushindwa kwa mbio hizo kutapimwa katika kipindi cha miezi na sio miaka. Amesema NASA itawekeza karibu dola bilioni 20 kwa kipindi cha miaka saba ijayo na kujenga kituo cha utafiti mwezini ambapo kutakuwa na safari kadhaa zitakazofanywa na wanaanga.

NASA ilitangaza mbinu ya ujenzi wa kituo hicho kwa awamu, ikisimamisha kwa muda kituo cha anga za juu cha Gateway kinachozunguka mwezi katika muundo wake wa sasa na kuelekeza malengo yake kwa miundombinu inayowezesha shughuli endelevu kwenye uso wa mwezi.

Kituo cha utafiti cha Gateway kilikuwa kimepangwa pamoja na Shirika la Anga za Juu la Ulaya (ESA) na kilikusudiwa kuwa kituo cha matumizi ya misheni za wanadamu kwenda mwezini na kwa misheni za kwenda Sayari Nyekundu au Mars.